Wakati Sayari Nyekundu Ilipokuwa Bluu
Jan. 17, 2013

Nafahamu unajua kuwa Dunia si sayari pekee katika Mfumo wa Jua na kuwa kuna sayari nane kwa ujumla. Lakini sayari inayofanana na Dunia kwa kiasi kikubwa ni Mars, ambayo imepewa jina la utani ‘Sayari Nyekundu’ kutokana na uso wake kuwa na rangi nyekundu. Kwa sasa inazidi kudhihirika kuwa sayari hii ya Mars ilikuwa ya bluu kwa mda mrefu hapo mwanzo, ikiwa na maziwa, mito na bahari zinazotiririsha maji, kama ilivyo kwa Dunia! 

Picha hizi za kupendeza zilipigwa na chombo cha Mars Express, ambacho kinaizunguka sayari ya Mars. Zinaonyesha mifereji ya mito ikikatiza katika uso wa sayari, inaaminika kuwa mifereji hii ilitengenezwa na maji yenye kina kirefu yaliyokuwa yanatiririka katika sayari hiyo katika miaka mabilioni iliyopita kabla hata ya binadamu kuwepo! 

Hata leo hii kuna maji katika sayari ya Mars, ingawa yameganda chini ya uso wa sayari katika vizio vya Kaskazini na Kusini (Kama Miamba ya Barafu iliyopo Duniani). Hivyo basi mifereji hii ya mito inaweza isionekane kama ni kitu cha kushangazak, ingawa ni mikubwa mno! Ikiwa na urefu wa kilometa 1,500, ambao ni urefu mkubwa kupita hata mto Rhine ambao unakatiza bara la Ulaya kutokea Uholanzi hadi Uswisi! Pia kina chake ni mita 300, ambacho ni kina kikubwa kupita mto wowote upatikanao Duniani! 

Picha hizi mpya kutoka katika chombo cha Mars Express zinatupa mtazamo mpya wa historia ya sayari nyekundu na kuifanya isionekane tofauti na dunia yetu ya leo! 

Dokezo

Wanasayansi wanaamini kuwa katika miaka mabilioni iliyopita sayari ya Mars iliathirika na mafuriko makubwa, ambayo hayajawahi kutokea katika historia ya mfumo wa Jua! Ni vigumu kutafakari kwa sasa, kwani siku hizi sayari ya Mars ina baridi kali sana, na tabaka lake la hewa ni jembamba sana kwa maji kuweza kutuama katika uso wake.

Mponda Malozo / UNAWE-Tanzania

Picha
Chapisha

Bado una shauku? Jifunze zaidi...

Space Scoop ni nini?

Vumbua astronomia zaidi

Hamasisha kikazi kipya cha wavumbua anga

Marafiki wa Space Scoop

Wasiliana nasi